dual citizenship

Pemba Paradise

Zanzibar Diaspora

Mwanakwerekwe shops ad

ZanzibarNiKwetuStoreBanner

ZNK Patreon

Scrolling news

************ KARIBUNI..................Contact us for any breaking news or for any information at: znzkwetu@gmail.com. You can also fax us at: 1.801.289.7713......................KARIBUNI

Monday, May 25, 2015

Gwajima, Flora Mbasha waibukia Chadema.

Askofu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima (kushoto) akizungumza kwenye mkutano wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Jimbo la Kawe, jijini Dar es Salaam jana na kulia mwimbaki wa nyimbo za injili, Flora Mbasha akiimba kwenye mkutano huo. PICHA TRYPHONE MWEJI
Askofu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima, jana aliibukia kwenye mkutano wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Jimbo la Kawe, Dar es Salaam.
 
Mkutano huo ulikuwa wa uzinduzi wa kitabu cha kazi alizofanya Mbunge wa jimbo hilo na Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake wa Chadema (Bawacha), Halima Mdee.
 
Askofu Gwajima alionekana kwenye jukwaa kuu na viongozi mbalimbali wa Chadema, akiwamo mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe, katika mkutano uliofanyika katika viwanja vya Tanganyika Packers, Kawe, jijini Dar es Salaam.
 
Miongoni mwa watu wengine  maarufu waliokuwapo kwenye mkutano huo ni mwimbaji wa nyimbo za injili, Flora Mbasha, ambaye aliimba wimbo maalum kwa ajili ya chama hicho na ulizinduliwa jana.
 
Mkutano huo ulitanguliwa na maonyesho ya kikundi cha ulinzi cha Chadema  (Red Brigade) na baadaye wimbo maalum wa amani na pongezi kwa chama hicho ulioimbwa na Mbasha na kuamsha shamrashamra kwa watu waliohudhuria ikiwamo kupanda jukwaani kucheza.
Mwenyekiti wa Chadema Taifa, Mbowe, akihutubia mamia ya wananchi wa jimbo hilo, alisema uchaguzi wa mwaka huu ndiyo matamanio ya baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Nyerere, ambayo alikuwa nayo wakati wa siku za mwisho za uhai wake.
 
“Mwalimu Nyerere alisema: “Watanzania wanataka mabadiliko, wasipoyapata ndani ya CCM watayatafuta nje ya CCM,” sasa wakati wa kuyatafuta nje ya CCM  umefika na Watanzania kwa kushirikiana na Ukawa na wananchi wasio na chama lakini wana mapenzi mema na nchi wanaungana nasi.”
 
Mbowe alisema baada ya kutembea nchi nzima amegundua Watanzania wanayataka mabadiliko, wana uwezo wa kuyaleta na wako tayari kuyaleta, utayari ambao hauipi amani CCM na kudai ndiyo maana ina haribu mfumo wa uandikishaji wapigakura katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kwa mfumo wa Biometric Voters Registration,” alisema.
 
AIPOPOA MAWE NEC
Alisema juzi alitembelea vituo vya uandikishaji mkoani Mbeya katika wilaya ya Rugwe Tukuyu, Kyela na alibaini Watanzania wanalala kwenye vituo vya kujiandikisha kwa sasabu vifaa havitoshi na imefanyika hivyo makusudi ili Watanzania wengi wasiandikishwe.
 
“Naomba kupitia mkutano huu nimshauri Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec), Jaji Damian Lubuva, lawama utakayoipata kutokana na BVR, CCM hawatakuwa na wewe, wanakutumia kwa sasa, kikiwaka utawekwa kando,” alitahadharisha na kuongeza:
 
“Vifaa (BVR Kits) havitoshi, tunakuomba (Jaji Lubuva) utangaze umeongeza siku za kujiandikisha na siyo siku saba ili wenye sifa wajiandikishe. 
 
“Nimeshuhudia kinamama wanalala vituoni kwa sababu uandikishaji umekuwa adhabu kwao,” alidai.
Mwenyekiti huyo wa Chadema ambaye pia ni Mwenyekiti wa Ukawa, alisema wapigakura wengi wanaunga mkono mabadiliko na wakijiandikisha itakuwa ni kaburi kwa CCM na kuongeza:
 
 “Jaji Lubuva kaburi ulilobeba ni lako mwenyewe, tunakuomba uongeze siku za kuandikisha wapiga kura.” 
Mbowe alisema uchaguzi mkuu kikatiba unatakiwa kufanyika Oktoba 25, mwaka huu na kwamba kwa sasa zimebaki siku 121 kufika siku hiyo na Nec haijatangaza majimbo ya uchaguzi na uwakilishi pamoja na ratiba ya uchaguzi.
 
“Wajiandae kisailokijia kuachia madaraka ya nchi, mnachelewesha uandikishaji wa wapiga kura ili wengi wasijiandikishe zimebaki siku chache utawala uliopo kwa sasa uondoke madarakani,” alisema Mbowe ambaye hotuba yale ilikuwa inarushwa moja kwa moja na kituo cha ITV.
 
Kwa mujibu wa Mbowe, serikali itakayoundwa na Ukawa itaongoza taifa katika misingi ya kurudisha utawala wa haki na sheria ili kurudisha matumaini kwa wananchi wote.
 
Aidha, aliwataka watumishi wa umma kutokuwa na hofu kwani Ukawa haingii kubadili au kufukuza mtu kazi, bali kufanya mabadiliko makubwa kwa Watanzania na kwamba kitakachobadilika ni vyama vinavyoongoza nchi na siyo mifumo ya utawala.
 
MISWADA YA HABARI 
Mbowe ambaye pia ni Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, alisema Mswada ya Sheria ya Huduma za Vyombo vya Habari na Muswada wa Sheria ya Haki ya Kupata Habari 2015, ikifikishwa bungeni mwaka huu, wabunge wa Ukawa watasimamisha Bunge na hawatakubali kuipokea.
 
“Ndani ya Muswada wa Sheria ya Huduma za Vyombo vya Habari uhuru wa kupata habari unataka ikifika saa mbili usiku, vyombo vyote vya habari binafsi ni lazima vijiunge na TBC One kusikiliza na kutazama taarifa ya habari, huu ni ukandamizaji na haikubaliki,” alisema huku akishangiliwa.
 
“Kupitia mkutano huu nawaambia siku serikali italeta miswada hiyo, tutasimamisha Bunge halitaendelea kwa sababu huwezi kufanya uporaji wa haki kwa kiasi hicho,” alisema. 
 
Aidha, alisema Muswada wa Sheria ya Makosa ya Mtandaoni 2015, uliopitishwa katika Mkutano wa 19 wa Bunge una vifungu visivyofaa na kwamba utawala utakaokuja hautaki sheria za kuminya uhuru wa watu na kwamba kama rais amesaini zitabaki ‘kapuni’ iwapo Ukawa wataingia madarakani.
 
Mbowe aliwataka wakazi wa jiji la Dar es Salaam kujiandikisha kwa wingi ili kufanya mabadiliko nchini kwa kuwa jiji hilo ndilo lenye wapigakura wengi.
 
Alisema licha ya kasi kubwa ya maendeleo na ukuaji wa jiji, lakini wananchi wanaishi maeneo ambayo hayajapimwa kwa kuwa marais watatu waliopita akiwamo Rais Jakaya Kikwete hawajafanya mipango miji na kwamba Mwalimu Nyerere alifanya ya kwanza wakati jiji likiwa na wakazi 275,000 na mara ya pili likiwa na wakazi 750,00.
 
Mwenyekiti huyo alisema kwa kasi ya ukuaji wa jiji na mpango wa ujenzi wa barabara za mabasi yaendayo kasi havilingani kabisa.
 
Kuhusu huduma ya majisafi na salama, alisema ni asilimia nane ya wananchi ndiyo wanaopata maji safi na salama, asilimia 80 wanatumia maji ya visima ikiwa ni miaka 51 ya Uhuru. Alisema jiji hilo ndiyo sehemu pekee ambako mtu anaweza kukaa kwenye foleni kwa saa sita, jambo ambalo linaonyesha utawala uliopo umeshindwa na nchi haiwezi kuendelea kwa kuwa na utawala wa aina hiyo. 
 
Mbowe alisema kuna dalili za wazi za serikali iliyopo kuchoka kwa kuwa kwa sasa kuna migogoro mikubwa baina ya serikali na madereva, watu wenye ulemavu, wanafunzi wa vyuo vikuu, wakulima na wafugaji.
 
ASKOFU GWAJIMA
Akizungumza na hadhara hiyo baada ya Mbowe kumaliza kuhutubia, Askofu Gwajima alisema hotuba ya Mbowe ina ujumbe mzito na kwamba ana amini aliyozungumza kaongozwa na Mwenyezi Mungu kuyazungumza kwa ajili ya umma.
 
Alisema anatambua kuwa Chadema ina thamini mabadiliko na kutoa baraka kwa chama hicho kuendelea na jitihada hizo kwa kuwa wakati wa ukombozi umewadia.
 
MNYIKA: WANAWAKE JITOKEZENI KUGOMBEA
Awali, Naibu Katibu Mkuu wa Chadema Bara, John Mnyika, aliwataka wanawake kujitokeza kugombea nafasi mbalimbali nchini katika uchaguzi mkuu ili kuongoza mabadiliko nchini kama alivyofanya Mdee katika jimbo hilo.
 
Alisema kinamama wana majukumu mengi, wanahangaika na shida katika huduma za afya, kuhudumia familia, kupata maji na mahitaji mengine muhimu ya familia, lakini wapo ambao wamejitokeza kwenye nafasi mbalimbali za uongozi na kufanya vizuri.
Mbunge Mdee akihutubia umati wa wananchi waliohudhuria, alisema alimkaribisha Mbasha Chadema na kwamba ni nyumbani kwa kuwa aliumia sana alipomkosa ndani ya chama hicho.
 
Aidha, aliwakaribisha wasanii wengine kujiunga na chama hicho kwa kujitokeza hadharani kama alivyofanya Mbasha.
 
Mdee aliwashukuru wananchi wa Kawe kumuweka katika ramani ya Tanzania na kwamba ni lazima kukiondoa Chama Cha Mapinduzi (CCM) madarakani kwa kuwa kimeshindwa kutekeleza mahitaji ya Watanzania.
 
Aidha, alisema wanawake wa Tanzania wanateseka kwa kukosa huduma muhimu za kijamii ufisadi umekithiri ndani ya serikali.
CHANZO: NIPASHE

No comments :

Post a Comment