dual citizenship

Pemba Paradise

Zanzibar Diaspora

Mwanakwerekwe shops ad

ZanzibarNiKwetuStoreBanner

ZNK Patreon

Scrolling news

************ KARIBUNI..................Contact us for any breaking news or for any information at: znzkwetu@gmail.com. You can also fax us at: 1.801.289.7713......................KARIBUNI

Saturday, October 21, 2017

Waziri Gavu: Msafara wa meli ya Sultan Qaboos hapa Zanzibar haihusiani na masuala yoyote ya kisiasa!

SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar imewaeleza wananchi wake kuwa ujio wa meli ya Sultan Qaboos hapa Zanzibar haihusiani na masuala yoyote ya kisiasa bali meli hiyo ilibeba ujumbe wa amani, kukuza ushirikiano na uhusiano uliopo kati ya Zanzibar na Oman.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Issa Ussi Haji Gavu, aliyasema hayo leo huko katika ukumbi wa zamani wa Baraza la Wawakilishi, Kikwajuni mjini Zanzibar wakati alipofanya mahojiano na waaandishi wa Habari wa vyombo mbali mbali vya Zanzibar na Tanzania Bara.Katika maelezo yake, Waziri Gavu alieleza kuwa katika kipindi chote cha siku nne cha kuwepo meli hiyo hapa Zanzibar ujumbe huo ulipata nafasi ya kukutana na viongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ambapo masuala mengi yaliyozungumzwa yakiwemo uhusiano uliopo pamoja na mashirikiano katika kuimarisha sekta za utalii, viwanda, elimu,uwekezaji, pamoja na mafuta na gesi.

Waziri Gavu alieleza kuwa katika ziara hiyo miongoni mwa mambo waliyokubaliana kati ya Serikali ya Oman na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ni pamoja na matengenezo makubwa ya jengo la Beit-el-Ajab, ukarabati mkubwa wa jengo la ‘People’s palace’, uwekezaji katika kiwanda cha kusindika samaki, uwekezaji katika kiwanda cha kutengenezea ‘juice’.

Jengine ni kuitangaza Zanzibar kiutalii na kuanzisha safari za moja kwa moja za watalii kati ya Zanzibar na Oman kwa wageni wa Oman wanaopendelea vivutio vya Zanzibar, kutoa msaada wa kiufundi na kisheria katika sekta ya mafuta na gesi kila inapohitajika kufanya hivyo pamoja na kutoa mafunzo ya muda mfupi na muda mrefu katika masuala ya mafuta na gesi asilia.

Aidha, Waziri Gavu alieleza kuwa wageni hao baada ya kufanya ziara yao hiyo katika visiwa vya Unguja na Pemba walikiri kuwepo maendeleo makubwa yaliofikiwa hapa Zanzibar kwani kati ya miongoni mwa wageni hao yupo alieza liwa katika Hospitali ya Mkoani Pemba na alishangwaza ilivyo hospitali hiyo hivi sasa na jinsi alivyoiacha yeye wakati huo.

Pamoja na hayo, ujumbe huo ulisifu amani, utulivu na mshikamano uliopo kati ya wananchi wa Zanzibar pamoja na kufurahishwa na mapokezi makubwa waliyoyapata kutoka kwa wananchi pamoja na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar hasa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein.

Pia, Waziri gavu alieleza kuwa hakuna Rais duniani anayefanya kazi kwa utashi wa mtu au kikundi cha watu ama kushurutishwa na kueleza kuwa uteuzi anaoufanya Rais Dk. Shein unatokana na azma ya kutaka mabadiliko katika kuiletea nchi maendeleo na anafanya kwa kuafuata sheria, taratibu pamoja na Katiba ya Zanzibar.

Waziri Gavu alitumia fursa hiyo kutoa shukurani kwa wananchi kwa ushirikiano, heshima na mapenzi makubwa waliyoyaonesha wakati wa hafla maalum ya kukabidhiwa na kufunguliwa ‘Masjid Jaamiu Zinjibar’ uliojengwa kwa mashirikiano na Serikali ya Oman chini ya uongozi wa Sultan Qaboos bin Said Al Said.

Sambamba na hayo, Waziri Gavu aliongeza kuwa kutokana na nchi mbali mbali duniani kuendelea kuiunga mkono Zanzibar, Ubalozi wa Saud Arabia unatarajia kufungua Ubalozi wake Mdogo hapa Zanzibar wiki ijayo.

Nae Mshauri wa Rais katika Ushirikiano wa Kimataifa, Fedha na Uchumi Balozi Mohammed Ramia Abdiwawa akijibu baadhi ya masuali yaliyoulizwa na waandishi waliohudhiria katika maojiano hayo, alisema kuwa uvumi wa kisiasa hauzuiliki hapa Zanzibar kwani kabla ya ujio wa meli, wakati meli ipo Zanzibar na baada ya kuondoka mambo mengi yamesemwa na kuzungumzwa na hasa kwa wale wasioipendelea mema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Balozi Ramia aliongeza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inakubaliwa na inaendelea kuungwa mkono na nchi mbali mbali duniani ikiwa ni pamoja na mashirika ya Kimataifa huku Rais wa Zanzibar akiendelea kupata mialiko kutoka sehemu mbali mbali duniani ambapo tayari baadhi yake ameshazitembelea na nyengine anatarajia kuzitembelea kuanzia mwaka ujao.

Hivyo, Balozi Ramia alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inafanya vizuri katika Nyanja za Kidiplomasia huku akisisitiza kuwa Zanzibar ina mahusiano mazuri na nchi za nje hivi sasa.

No comments :

Post a Comment